FAHAMU KILIMO BORA CHA MPUNGA CHA UMWAGILIAJI
Maandalizi sahihi ya shamba ni jambo la msingi katika kuboresha kilimo cha umwagiliaji wa mpunga. shamba lisipoandaliwa vema husababisha mbinu bora zinazoshauriwa kutoonyesha matokeo katika kiwango kinachotarajiwa hasa katika
uzalishaji. Kimsingi maandalizi ya shamba yanatakiwa yafanyike kwa usahihi
na kwa wakati katika mtiririko unaotakiwa. Zifuatazo ni hatua saba muhimu na za msingi katika kilimo cha mpunga
1. KUSAFISHA SHAMBA
Safisha shamba mapema kabla ya msimu kuanza. Kusanya na kuangamiza visiki na takataka
nyingine zote. Masalia ya mazao yanaweza kutumika kutengeneza mbolea ya mboji. Inapobidi tumia moto kwa uangalifu sana maana moto unaweza kuharibu mazingira, unaua wadudu rafiki, unaharibu udongo na kuteketeza mboji.
2. KULIMA
Kulima husaidia kupunguza kiasi cha magugu, huruhusu mzunguko mzuri wa hewa na maji, hurahisisha mizizi kupenya na
kuchanganya masalia ya mazao kwenye ardhi. Wakati wa kulima uangalifu unahitajika ili kuzuia kuharibu
usawa wa ardhi. Kina cha kulima kiwe kati ya sentimeta 10 na 15. Ili
kurahisisha na kuharakisha kazi ya kulima ni vema kutumia zana/mashine rahisi
kama Trekta la mkono na wanyamakazi
3. KUKARABATI/KUJENGA MAJARUBA
Baada ya kulima hakikisha kuwa kingo za jaruba zimekarabatiwa ili kuweza kuhifadhi maji vema. Kama ni shamba jipya, ujenzi wa kingo za jaruba ufanyike kwa kufuata utaalamu unaotolewa. Kingo imara ni muhimu kudhibiti vema maji shambani.
4. KUVURUGA
Weka maji shambani kiasi cha sentimeta 3 hadi 5 juu ya usawa
wa ardhi ili kukamilisha vema uvurugaji. Jembe la mkono linatumika lakini ili kurahisisha na kuharakisha kazi hii ni vema kutumia trekta la mkono au wanyamakazi. Unapotumia wanyamakazi au trekta la mkono weka maji shambani si zaidi ya siku moja kabla. Shamba lililovurugwa vema huiwezesha mizizi ya miche kupenya vema ardhini.

